Rais wa Zanzibar na
Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dkt Hussein Mwinyi leo amewaongoza
waombolezaji wakiwemo viongozi na wananchi kwenye mazishi ya aliyekuwa Makamu
wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Sharif Hamad.
Mazishi ya Maalim
Seif ambaye pia alikuwa Mwenyekiti wa Chama cha ACT Wazalendo yamefanyika
kijijini kwake Mtambwe katika wilaya ya Wete visiwani Pemba
Kabla
ya mazishi hayo, mwili wa marehemu maalim Seif uliswalia kwenye uwanja wa
Gombani na kabla ya hapo pia katika msikiti wa Maamur jijini Dar es salaam
pamoja na viwanja vya Mnazi Mmoja mjini Unguja.
Katika
mahali ambapo mwili huo ulipita, maelefu ya waombolezaji walijipanga barabarani
na kwenye viwanja ambavyo kulikuwa na swala ili kutoa heshima zao za mwisho kwa
kiongozi huyo ambaye ametajwa kama nguzo muhimu ya umoja na mshikamano wa
kitaifa.
Akitoa
salamu za chama, Kiongozi Mkuu wa ACT Wazalendo Zitto Kabwe, amesema maalim
Seif aliyaishi yale yote aliyoamini na kuwaasa viongozi wengine na vijana kuiga
mfano wake na kuahidi kwamba chama cha Act kitayatimiza maono yake na kutoa
ushirikiano unaohitajika kwa serikali ya Umoja wa Kitaifa Zanzibar.
“Wengi
mnafahamu kwamba mimi si mtu wa kukosa maneno, lakini leo nakosa maneno ya
kumwelezea Mwenyekiti wangu Maalim Seif Sharif Hamad - nakosa maneno kwasababu
Maalim mwenyewe ni maneno,” amesema Zitto.
Chama cha ACT Wazalendo kitakuwa na wajibu wa kuhakikisha kuwa kinampata Mrithi Maalim Seif ndani ya kipindi wiki mbili.
Wengi mnafahamu kwamba mimi si mtu wa kukosa maneno, lakini leo nakosa maneno ya kumwelezea Mwenyekiti wangu, nakosa maneno kwasababu Maalim mwenyewe ni maneno
- Zitto Kabwe
Faraj Faridhi ni
mchambuzi wa masuala ya kisiasa ambapo anasema kuwa kuna ugumu wa kuliziba
pengo la Maalim Seif katika siasa za upinzani kutokana na uwezo wake mkubwa wa
kuthamini utu na haki za watu.
“Maalim
Seif Sharif Hamad ikumbukwe alikua na misimamo ya kutaka utu wa mtu usipotee au
haki ya mtu isipotee, lakini katika siasa za Zanzibar, tumeona tangu mwaka 1995
kwa chaguzi zote mpaka 2020 kulikua hakuna mgombea wa upinzani mwenye nguvu wa
kumfikia Maalim Seif na pia ikumbukwe siasa za Zanzibar ni mtu na mtu mwenyewe
ni Maalim Seif Sharif Hamad,” amesema Faridhi
Maalim Seif amefariki dunia Februari 17 asubuhi katika
Hospitali ya Taifa ya Muhimbili alikolazwa tangu Februari 9 kwa matibabu.
Leave a comment